SEXUAL SADISM

Sexual Sadism, yaani maradhi ambayo aliyenayo huona raha mtu wa jinsia tofauti na yeye anapodhalilika au kuteseka kijinsia.

Sexual Sadism ni maradhi ambayo yanawapata wake kwa waume, ingawaje maradhi haya hukithiri kwa wanaume.


Mara nyingi wanaume wenye maradhi haya hutumia nguvu za kimaumbile au za kiutawala kuwadhalilisha wanawake kijinsia. Hawa huona raha wanapowadhalilisha wanawake kwa njia mbalimbali kama vile kuwashikashika bila ya ridhaa yao, kuwaangalia kwa jicho la fitna, au kuwatolea lugha za kejeli na kuwaita majina yasiyofaa. Wengi katika hawa hufikia hatua ya kuwabaka wanawake kwa kuwakomoa tu au kuwadhalilisha, au ukomo wa raha yao huja pale wanapomfanyia mwanamke jambo linalomuudhi au kumuumiza. Hili ni kundi la wagonjwa mahututi.


Kundi jingine ni la wanaume ambao, japo hawashiriki moja kwa moja katika udhalilishaji, hufurahia mwanamke anapodhalilika au kudhalilishwa kijinsia. Hawa husifia vitendo vichafu walivyofanyiwa wanawake, na huona waliofanya hivyo ndio wanaume. Mara nyingi unaweza ukawakuta vijana wahuni wakipongezana na kuwahadithia wenzao kwa ushabiki na furaha jinsi mwanamke fulani alivyodhalilishwa kijinsia, kwa kubakwa na kundi la wanaume, au kufanyiwa tendo lolote la kinyama na kihayawani.


Mfano mwingine wa watu wenye maradhi haya ni wale wanaoshangilia kuona mwanamke anadhalilika kijinsia, labda kwa bahati mbaya. Kwa mfano, mwanamke anaweza kujikwaa na kuanguka kiasi cha kuonekana baadhi ya sehemu za siri na utakuta kundi la vijana (na wengine watu wazima) wakitoa mayowe na vifijo, wengine wakipiga miluzi kushabikia yaliyotokea.


Au mfano mwingine ni pale labda mwanamke mgonjwa wa akili anapovua nguo na kutembea wazi, panapotokea wasamaria wema kumhifadhi utakuta wenye maradhi haya ya Sexual Sadism hukasirika wakilaumu kuwa wameondolewa sinema ya bure.


Wapo wanawake vile vile wenye maradhi haya, japo wao mara nyingi hawawezi kutumia mabavu kuwadhalilisha wanaume. Baadhi yao ni wale ambao hujitoa nje katika hali ambayo wanajua kwamba wanaume watakao waangalia watateseka kimaumbile. Hawa ni wendauchi ambao kwa makusudi hutumia maumbo yao kuwatesa wanaume majiani na mabarazani.


Wendawazi hawa vile vile ni chanzo cha matukio mengi ya ubakaji, kwani wanaume wengine hushindwa kuendelea kuvumilia hali iliyosababishwa na uvaaji na uchochezi wa mwendawazi yule. Hivyo wabakwao wengi huanza kuwabaka wabakaji kisaikolojia. Jamii ya Kiislamu husalimika na maradhi haya kwa kusisitiza stara (hijab) kwa wanawake na wanaume.


Ama suala zina la ugonjwa huu wa Sexual Sadism kunakuwa hakuna dawa kwa jamii kama hii yetu, yenye mfumo wa maisha wa kikafiri (kufru culture) ambapo hakuna sheria inayoongoza mahusiano ya wanaume na wanawake. Kila mmoja anadai uhuru wa kujiamulia mambo, kwa hiyo uhuru huo umetoa mwanya kwa wadhalilishaji kuwa huru kuwadhalilisha wenzao. Uislamu pekee ndio kinga dhidi ya Sexual Sadism na maradhi kama hayo.


Jambo la kwanza, Uislamu hauruhusu michanganyiko ya holela ya wanaume na wanawake wasio ndugu. Hii hupunguza fursa (opportunity) ya watu wa jinsi tofauti hata kuongea, zaidi ya salamu ya amani.


Pili, Uislamu unamtetea mwanamke hata anapokuwa amesingiziwa tu kuwa amefanya uovu. Msingiziaji hutakiwa apewe adhabu ya viboko themanini vya nguvu


Na wanao wasingizia wanawake mahashumu, kisha wasilete mashahidi wane, basi watandikeni bakora thamanini, na msiwakubalie ushahidi wao tena. Na hao ndio wapotovu.

(Qur’an 24:4).


Tatu, Sheria ya Kiislamu ina adhabu kali dhidi ya wazinifu. Leo hii wadhalilishaji ni wengi kwa vile uzinifu umepewa leseni na umekuwa sio dhambi. Lakini kama wazinifu wangekomeshwa, wadhallishaji, wenye maradhi ya Sexual Sadism wangetokea wapi?


Nne, wanawake na wanaume wamekatazwa hasa kudhalilishana.

Enyi mlio amini! Wanaume wasiwadharau wanaume wenzao, wala wanawake wasiwadharau wanawake wenzao. Huenda hao wakawa bora kuliko wao. Wala msivunjiane hishima, wala msiitane kwa majina ya kejeli. Ni uovu kutumia jina baya baada ya kwisha amini. Na wasio tubu, hao ndio wenye kudhulumu.

(Qur’an 49:11)


Tano, Uislamu unakataza hata kukodoleana macho yanayoweza kuleta fitna, kwa kuwaambia wanaume na wanawake washushe macho yao chini…


Waambie Waumini wanaume wainamishe macho yao, na wazilinde tupu zao. Hili ni takaso bora kwao. Hakika Mwenyezi Mungu anazo khabari za wanayo yafanya.

(Qur’an 24:30)


Sita, Uislamu umemtaka mwanamke ajihifadhi. Katika Uislamu mwili wote wa mwanamke ni uchi, isipokuwa uso na viganja. Hivyo mwanamke wa Kiislamu hawezi kuwadhalilisha wanaume, na ni vigumu kwake kudhalilika:


"Ewe Nabii! Waambie wake zako, na binti zako, na wake za Waumini wajiteremshie nguo zao. Hivyo ni karibu zaidi kuweza kutambulikana wasiudhiwe. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu."

(Qur’an 33:59)


Kwa ujumla, jamii kufuata Uislamu ni kusalimika na kila janga la ulimwengu huu, hasa yale yanayo sababishwa na sisi wenyewe kwa matendo yetu. Hivyo janga la kudhalilishana kijinsia vile vile litaondoka kwa kufuata sheria za Kiislamu.

0 comments/Maoni: